Sababu za vijana wengi kutofikia malengo ya uongozi zatajwa

 


Na Tallib Ussi Hamad

 

Wakati Dunia ikiendelea kupiga hatua zaidi kushirikisha vijana wengie katika nafasi mbali mbali za uongozi inaelezwa kuwa visiwani Zanzibar hali ya ushiriki wa vijana katika nafasi za maamuzi bado haijaridhisha.

Kulingana na matakwa ya Umoja wa Mataifa unamtafsiri kijana ni mtu aliye baina ya umri wa miaka 15 na 24. Na, kwa mujibu wa Sera ya Maendeleo ya Vijana Zanzibar, kijana ni mtu mwenye umri kuanzia miaka 15 hadi 35. Kulingana na sensa ya watu na makaazi ya mwaka 2012, Zanzibar ina idadi ya watu 1,303,569 ambapo kati yake wanawake ni 672,892 sawa 51 na wanaume ni 630,677 sawa na 49. Katika idadi hiyo, vijana walikadiriwa kufikia 456,249 ambao ni sawa na 35%. Miongoni mwao vijana wa kike ni 232,687.

Katika mkutano wa hivi karibuni ulioitishwa na TAMWA-ZNZ na kuwashirikisha wadau mbali mbali vijana wa vyama vya siasa na wasomi wa vyuo vikuu ulibaini uwepo wa mazingira yasiokua rafiki kwa vijana zaidi jinsia ya kike na ndio miongoni mwa sababu kushindwa kufikia malengo yao.

Wakati akichangia katika mkutano huo Dkt,Nassra Nassor alisema Kubaguliwa kwa watoto wa kike  katika mambo mengi kwa sababu tu ya kuwa kwake mwanamke kumekua kukiwadumaza wanawake kiakili na kuwafanya kudhani wao si sehemu ya jamii wanayopaswa kuwa viongozi badala yake hubaki nyuma tangu wakiwa wadogo mpaka wanapokua wakubwa.

Alisema changamoto hizo za kifamilia huwafanya wanawake kuonekana  ni wapiti njia mpita njia kwenye  familia yake na familia kumuonesha kuwa wao wanapaswa kusubiri kuolewa tu.

Kwa upande wake mwanaharakati na mwanasiasa kijana kutokea CHADEMA Zeudi Stephano alisema haki ya kupata elimu licha ya kuwa ni miongoni mwa haki muhimu za kikatiba lakinin bado kwenye familia nyingi hadi sasa wamekua wakishindwa kutoa usawa kwa watoto wakike na wakiume na wapo baadho ya wazazi ambao wamekuwa wakiwekeza nguvu zao zaidi kwa watoto wa kiume kwenye elimu huku wakiwadumaza watoto wa kike na kuwafanya wao kutokua sehemu ya watu wanaopaswa kupata elimu ya kutosha.

Sambamba na hayo mazingira ya ugawaji wa majukumu kwenye familia nyingi ni sehemu ya tatizo jengine ambao huwafanya wanawake wengi kushindwa kuwa viongozi kwani wanawake wengi kwenye familia hupewa majukumu makubwa zaidi kuliko wanaume na kujikuta muda mwingi wanatumia kufanya kazi baada ya kujisomea.

Nae Mkurugenzi wa  TAMWA-ZNZ Dkt,Mzuri Issa alisema wamebaini  kuwa suala la ulizi wa kupitiliza kwa watoto wa kike limekua likidumaza akili zao na kuwafanya kubaki na mawazo mgando kutokana na kukosa fursa ya kuchanganyika na wenzao ambapo tunaamini wangeweza kusoma mambo mapya na ya msingi kwa mustakbali wa maisha yao.

Hata hivyo alisema licha ya uwepo wa mazingira ya aina hiyo bado swangependa kuwakumbusha vijana bado ushiriki wao katika nafasi za uongozi ni muhimu kwa kuwa ni miomgoni mwa wadau muhimu wa maendeleo na tunapaswa kuendelea kuchukua juhudi mbalimbali ili kuwezesha ushiriki mpana katika maendeleo ya nchi yetu.

Comments